Decoration & Catering Services

Decoration & Catering Services

Boutique

Boutique

Tuesday, August 6, 2013

Hatimaye John Tendwa, out!

Rais Jakaya Kikwete amemteua Jaji Francis Mutungi kuwa Msajili wa Vyama vya Siasa kujaza nafasi iliyoachwa na John Tendwa ambaye amestaafu kwa mujibu wa sheria.
Taarifa iliyotolewa Dar es Salaam jana na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue ilisema kuwa uteuzi huo ulianza Agosti 2, 2013.
Kabla ya uteuzi huo, Mutungi ambaye ameshika nyadhifa mbalimbali katika idara ya Mahakama, alikuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma.
Alikotoka
Historia ya Jaji Mutungi katika utumishi wake mahakamani ilianza mwaka 1989 alipoanza kazi akiwa hakimu, baadaye akateuliwa kuwa Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.
Baadaye aliteuliwa na kushika nafasi za Msajili Mahakama ya Ardhi; Hakimu Mfawidhi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Msajili Mahakama ya Rufani na hatimaye Jaji katika Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma.
Kuhusu Tendwa
Tendwa ameachia nafasi hiyo akiwa katika msuguano wa kisiasa na baadhi ya vyama vya siasa, kikiwamo Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) ambacho hivi karibuni kilitangaza kutokumtambua wala kushirikiana naye.
Katika utumishi wake huo wa miaka 12 tangu alipoachiwa nafasi hiyo na Jaji George Liundi, Tendwa amekuwa akishutumiwa mara kwa mara kwa upendeleo dhidi ya vyama vya upinzani, madai ambayo amekuwa akiyapuuza. Alipotafutwa tena jana kuzungumzia madai hayo hakupatikana kwa kuwa alikuwa nje ya nchi.
Mbali na Chadema, Tendwa ambaye amewahi kukwaruzana na vyama cha CUF na TLP, mara nyingine amekuwa akitoa tishio la kuvifuta vyama hivyo kwa kile alichodai kuwa vinachochea vurugu.
Hali hiyo ilimjengea uhasama baina ya ofisi yake na vyama vya upinzani na kuna wakati aliwahi kutajwa adui namba moja wa vyama vya upinzani na demokrasia.

0 comments:

Post a Comment