Decoration & Catering Services

Decoration & Catering Services

Boutique

Boutique

Sunday, November 10, 2013

ANA kwa ANA: Nyota mbovu, msanii mwenye vipaji lukuki.

Masai Nyota Mbofu


Na Gadiel Frank Mpungu.

Wamasai ni moja kati ya makabila makubwa barani Afrika ambapo lenyewe lipo katika zaidi ya nchi moja. Mavazi yao pamoja na mtindo wa kuhama hama makazi kutokana na kufuga ni sifa zinazo zidisha umaarufu wa kabila hili.

Giliady Severine ni mchekeshaji (comedian), kazi ambayo imempa jina kubwa hapa nchini na kumfanya akubalike sana. Lafudhi anayoitumia msanii huyu katika kazi zake, ni ile ya Wamasai huku akivalia na mavazi ya watu wa kabila hilo.

Giliady ambae wengi wanamfahamu kama Nyota Mbovu au Nyota Mbofu nimzaliwa wa Ujiji, Kigoma na kwasasa ana umri wa miaka thelathini na mitatu.

Nyota Mbovu anasema kuwa watu wengi wanaamini kuwa yeye ni mmsai kutokana tu na kuuvaa vilivyo uhusika wa kabila hilo. Aidha amesema kwamba si watu wa makabila mengine tu wanaoamini kuwa yeye ni mmasai, bali hata Wamasai wenyewe wanaamini kuwa yeye ni ndugu yao na hata kufikia hatua ya kumsemesha kilugha pindi wamuonapo.

Mchekeshaji huyu amethibitisha kuishia kidato cha tatu nchini Kenya mwaka 1998 na kusema kuwa diesel iliishia njiani na kama ingalikuwa ni meli ingalizama baharini. Baada ya kuacha shule, Nyota Mbofu alijihusisha na uchimbaji wa madini ya Tanzanite tangu mwaka 1998 hadi mwaka 2001.

Nyota amesema katika maisha yake hakuna kazi nyingine yoyote anayoitegemea zaidi ya sanaa huku Vituko sanaa group kikiwa ndicho kikundi cha kwanza kabisa  Nyota Mbofu kukitumikia katika sanaa.

Katika maongezi yake na Blog hii Giliady amekiri kuwa, aliwahi kufanya yale maonyesho ya barabarani ambayo ameyaita kuwa ni maonyesho ya utalipa ukipenda mwenyewe, kiingilio utajua mwenyewe.

Pamoja na hayo amesema kwamba alishashiriki sana maonyesho ya mashuleni na kuongeza kuwa, yalikuwa na changamoto nyingi ikiwemo wanafunzi kuja na fedha pungufu au kuja hata na mayai au maparachichi badala ya pesa.

Mchekeshaji huyu ambaye ameonekana kuwa mwenye furaha sana wakati akiongea na blog hii, amesema aliamua kuigiza kimasai kwa kuwa hapakuwepo msanii yeyote aliyekuwa anaigiza kwa kutumia lafudhi na mavazi ya kabila hilo, zaidi ya marehemu Ebo aliyekuwa ni mwanamuziki.

 Zaidi ya hilo Nyota Mbofu anasema kuwa aliona kabila hili lipo katika nchi nyingi barani Afrika tofauti na makabila mengine yaliyopo hapa nchini, kigezo ambacho anaamini kuwa kitamsaidia kukubalika hata akienda huko.

Masai amesema mpaka sasa ana nyumba ya kiasi cha shilingi milioni kumi na sita, ikiwa ni ya vyumba viwili iliyoko Chanika, wilaya ya Temeke. Lakini kabla ya kuwa na nyumba  hiyo ambayo ameiita sehemu ya kujificha, Masai anakiri kuwa alishawahi kupata usumbufu sana katika nyumba za kupanga hususani tangu alipoanza kuonekana kwenye runinga. 

Rungu na mkuki ni nyimbo ambayo imemtambulisha mchekeshaji huyu katika ulimwengu wa muziki ambapo amesema kuwa aliamua kuingia katika tasnia hii ili kuzidi kuonyesha kipaji chake cha sanaa na pia kujiongezea mashabiki. Suala ambalo amesema kwamba limefanikiwa kwa kiasi fulani kwani hata waandaaji wa kazi zake za uchekeshaji, kwasasa wanamlipa vizuri zaidi kutokana na umaarufu anaoendelea kujizolea katika muziki. 

Vilevile Nyota Mbofu amesema kwamba mpaka sasa ana nyimbo tatu zikiwa ni Yero suvai ambayo amefanya na Rich Mvoko pamoja na Kitokololo, Tipwa tipwa pamoja na nyimbo hiyo iliyomtambulisha katika muziki.

Akizizungumzia nyimbo hizo, Giliady amesema kuwa Rungu na mkuki ni nyimbo inayo zungumzia kazi ya ulinzi pamoja na changamoto zake.Yero suvai ikiwa ni nyimbo inayo uelezea utamaduni wa Wamasai huku Tipwa tipwa, ikimzungumzia mwanamke mnene na tabia zake.

Kitu kilicho muumiza sana msanii huyu hata asikisahau ni kifo cha marehemu mama yake. Ambapo Nyota Mbovu amesema kwamba namna alivyofikishiwa ujumbe huo haikuwa nzuri kwani alipigiwa tu simu na kuambiwa “mama yako kanyongwa” amesema Nyota Mbofu na kuongeza kuwa aliishiwa nguvu ghafula na kuketi barabarani alipokuwapo wakati huo.

Kitu kilichowahi kumfurahisha sana rafiki, ni pale alipofanikiwa kuonekana kwenye runinga kwa mara ya kwanza, akiwa katika kikundi cha Jakaya Theatre Art.
Suala la haki za wasanii kwa Nyota Mbofu halimuhusu sana kwani amesema kuwa hajawahi kuwa chini ya mtu yoyote tangu aanze sanaa. Hivyo labda mpaka asimamiwe kazi zake ndipo atajua kama wasanii hupunjwa fedha zao au ni maneno tu.

Akiliongelea suala zima la mahusiano, Masai amesema kwamba alishawahi kuumizwa sana na wasichana ambao wengi wao hudhani kuwa mtu kama yeye huwa na pesa nyingi, maghorofa kadhaa na magari, jambo ambalo Masai amekiri si la kweli. Masai aliongeza kuwa baada ya kugundua ukweli, huanza kupunguza mapenzi taratibu na kwenda kwa wale wenye maslahi kwao. 

Aidha baba huyu wa mtoto mmoja ambaye alizaa na msichana mwenye tabia hiyo aliyoisema hapo juu, amesema kuwa hajui ataoa lini na inatokana na yeye kuwa na bahati mbaya ya kupata wasichana ambao si Wakristo, jambo ambalo anasema huzua utata kila wafikiriapo suala la ndoa.

Vilevile Nyota Mbofu ameweka wazi kwamba alishawahi kuwa na mahusiano na wa mama watu wazima, akiwa na imani kuwa angetoka kimaisha jambo analokiri kuwa halina ukweli ndani yake na kwamba ulikuwa ni utoto. 

Giliady amesema kuwa yeye ni mzima na ameshawahi kupima magonjwa mengi likiwemo lile la Ukimwi.
Lakini anaelezea kwamba aliamua kupima VVU kwa mara ya kwanza kwani kwa kipindi hicho alikuwa na mpenzi aliyesemekana kuwa muathirika. Yeye na mpenzi wake huyo walishauriana na kuamua kwenda kupima afya zao na yeye akaonekana kuwa mzima, huku yule binti akiwa kweli ni muathirika. 

Hata hivyo Nyota Mbovu anakiri kuwa aliumizwa sana na taarifa hizo, kwani walipendana sana.

Mchekeshai huyu amekiri kuwa haamini kabisa katika ushirikina na kwamba yeye ni muoga sana wa mambo hayo japo anao marafiki ambao ni waumini wazuri wa imani hizo. Giliady anaongeza kuwa kama ingekuwa kutoka ni lazima ushiriki mambo hayo ya ushirikina, basi yeye asingefika hata alipo sasa.

Bambo ndiye msanii pekee anaye mvutia sana Masai ambapo mwenyewe amelithibitisha hilo na kusema mara nyingine hata Bambo asipochekesha, huwa anacheka tu kwa kuwa anamkubali sana.

Giliady anasema kuvutiwa kwake huko, kulimsababisha yeye kuiiga sauti ya msanii huyo hapo mwanzoni na hata kufikia hatua ya kuitwa Small Bambo huko mkoani Kilimanjaro.
Masai amethibitisha kutoipenda na wala kutofuatilia kabisa siasa ya hapa nchini.

Mavazi na mtindo wa nywele za Nyota Mbovu anasema ni  tshirt na jeans kwani akivaa suruali ya kitambaa na shati ni kama ameangukiwa na muamvuli, pamoja na rasta ambazo huamini kwamba humpa upekee.

Matarajio ya msanii huyu katika sanaa yake ni kuwa na nyimbo zenye mvuto zaidi kwa jamii pamoja na kupanda kiwango katika uchekeshaji.

Vilevile anatamani kuwa na uwezo wa kuwakusanya wasanii wa vichekesho na kufanya nao kazi mbalimbali kama wafanyavyo sasa yeye na wachekeshaji wenzake, chini ya kampuni moja ya hapa nchini.

Nyota Mbovu anaomba jamii izidi kumkubali, kumfuatilia na kuzipenda kazi zake na kuongeza kuwa anawaomba sana wasichana watoe Ukimwi na si mimba japo hana uwakika kama utatoka, yakiwa ni maneno yake ya mwisho kati yake nami.

0 comments:

Post a Comment