Decoration & Catering Services

Decoration & Catering Services

Boutique

Boutique

Sunday, November 10, 2013

MAKALA: Sanaa iliyopigwa teke hapa nchini.




 graffiti

 graffiti

 Na Gadiel Frank Mpungu.

Graffiti ni moja kati ya kazi za sanaa ambayo kwasasa imeshika hatamu katika sehemu mbalimbali duniani kote na hata nchini kwetu pia ambapo nayo hufanya kazi zilezile za kuelimisha, kuburudisha, kuonya na hata kupinga mambo mbalimbali katika jamii kama ilivyo kwenye sanaa zilizo zoeleka. 

Neno Graffiti kwa asili ni kutoka kule Ureno ambapo lina maana ya mkwaruzo.Wasanii wa kipindi hicho waliokuwa wakiutumia mtindo huu walihitaji mawe,chokaa na miti ili kuweza kuchora michoro yao na kufikisha jumbe zao kwa jamii.

Aidha wanagraffiti hutumia mtindo ule ule wautumiao wasanii wengine haswa wachoraji, wa kutoa mawazo akilini na kuyapeleka katika karatasi kwa kutumia mikono yao ambapo wao huchora maumbile mbalimbali na kuandika jumbe tofauti tofauti zenye kugusa jamii katika kuta, na si karatasi au canvas kama wengine. 

Mawazo, rangi na ukuta ndivyo vitu pekee kwasasa vinavyo hitajika katika sanaa hii ili kufikisha ujumbe katika jamii. Rangi zinazotumika kuchorea michoro ya graffiti hujulikana kama Spray cane (makopo ya kunyunyiza) ambapo wataalamu wanasema kuwa rangi hizi zinaupulizaji wake ili kuweza kutoa umbile sahihi la kitu unachotaka kukichora ukutani.

Changamoto ni zilezile kama ilivyo katika sanaa zingine ambapo wanagraffiti wamelalamikia uhaba wa rangi ambazo ndizo muhimu sana ili msanii aweze kufanikisha kazi yake pamoja na mambo mengine mengi likiwemo suala zima la kukosa wateja kutokana na kile walichokiita kuwa ni kutotambulika sana kwa kazi yao hiyo hapa nchini.

Vijana wa sasa ndilo rika pekee linaloonekana kuvutiwa sana na aina hii ya sanaa aidha kutokana na ile imani ya usasa au tabia ya mazoea ya kitu fulani ambayo watu wenye umri mkubwa wamekuwa nayo na hapa wao huwa na mazoea ya aina fulani ya sanaa. Hata hivyo wasanii wenyewe wa graffiti au waweza kuwaita wanamikwaruzo ukitumia maana halisi ya neno graffiti, wengi ni vijana ambao kwa ujumla wao huwa na mawazo mengi akilini yakiwemo yale ya kimapinduzi katika nyanja mbalimbali za maisha ya binadamu.

Japo kuwa sanaa hii imeonekana kuwa ya kisasa zaidi kwani hata malighafi zake hutumika zile za nje ya nchi kwa maana ya rangi, lakini nayo inaaminika kuwa ni kati ya sanaa zenye usiri katika baadhi ya jumbe zake zifikishwapo kwenye jamii. Usiri huo upo katika ubunifu wa michoro na maandishi ambayo msanii huyatumia, ili kutoa yale ya moyoni ambapo kwa mara kadhaa sasa unakuta msanii anachora michoro migumu au maneno yake kuyaandika nje ya utaratibu uliozoeleka jambo linaloweza kuleta shida katika uelewaji wa ujumbe.

Lakini swali ni je, ni kwanini basi sanaa hii hufanywa katika ukuta, treni, magari na sehemu nyinginezo zinazoonekana kwa uwazi zaidi na si kwenye canvas au karatasi?

Wachata Crew ni moja kati ya makundi maarufu sana hapa nchini katika sanaa hii ya graffiti. Aidha kundi hili lenye watu sita lililoanza rasmi mwaka 2007, limefanikiwa kuifanya kazi hii kwa miaka sasa ambapo limejizolea umaarufu mkubwa ndani ya nchi na hata kuipeperusha vyema bendera yetu nje ya mipaka ya Tanzania. 

Local na Kalasinga ndiyo wawakilishi wa WCT yaani Wachata Crew Tanzania katika mahojiano yaliyofanywa na Sherehe juu ya sanaa hii, ambapo wote walisema kuwa sanaa hii imekuwa ikifanywa ukutani na hata sehemu nyingine za kuonekana zaidi kama kwenye treni na kwingineko, ili tu ujumbe wa msanii uweze kufika kwa urahisi katika jamii ikiwa ni pamoja na kuonekana kwa watu wengi zaidi.

Akifafanua kwa undani juu ya hilo, bwana Local amesema kuwa kwenye miaka ya 1960 msanii Tack one83 ndiye aliye uanzisha mtindo huo wa kuchora katika sehemu za uwazi na kuitambulisha vyema sanaa hii ya graffiti kwa kutumia Spray cane kule nchini Marekani katika jimbo la Newyork,. Aidha Local aliongeza kuwa, msanii huyo aliweza kuchora michoro mingi sana kwenye kuta na hata kwenye treni akiwa na lengo moja kuu la kufanikiwa kuwafikia watu wengi zaidi katika kila ujumbe aliyoutoa kupitia sanaa yake hiyo.

Hata hivyo baada ya wanagraffiti wa huko Marekani kuonekana kuchafua mazingira na kuta za watu, serikali iliamua kuihesabia sanaa hii kama moja kati ya makosa ya kimazingira na kuwapa adhabu wale wote waliokutwa wakiifanya pasipo vibali rasmi vya wamiliki wa maeneo husika.

Hali hii iliwapelekea wasanii wa graffiti kwenda mbali zaidi na kuanza kuzifanya kazi zao kwenye kuta za ndani kwa wale wamiliki wa nyumba na maofisi waliyopenda yaani In door, ambapo kwasasa waliitumia sanaa hii pia kama njia ya kujipatia kipato.

Hata hivyo bwana Local alipozungumzia suala la graffiti kufanywa kwenye canvas au kuta za ndani alisema kuwa ni kuibana graffiti kwani lengo haswa ni kuonekana kwa watu wengi zaidi pasipo gharama yoyote ya kifedha ama muda ambao unaweza kutumika ili kwenda kuiona katika gallery kama ilivyo kwenye sanaa nyinginezo.
Suala la uchoraji wa vitu vilivyo nje ya tamaduni na maadili yetu au uandishi wa matusi kwa kupitia sanaa hii ni moja kati ya vitu ambavyo WCT wakiwakilishwa na Local na Kalasinga waliweza  kuviongelea pia, ambapo Kalasinga alisema kuwa huo ni ukosefu wa nidhamu ya kazi hiyo kwani hakuna sehemu yoyote inayo mruhusu mwanagraffiti kufanya mambo hayo.
Akiongeza juu ya hilo bwana Kalasinga alisema kuwa jambo lingine ni ukosefu wa elimu juu ya sanaa hiyo na kuwa, watu hudhani kuwa kila mtu anaweza kufanya graffiti na kutoa kile kilichopo akilini mwake alimradi tu aweze kupuliza lile kopo lenye rangi jambo ambalo si sahihi kwani sanaa hii nayo ni kazi na ina miiko kama zilivyo kazi nyingine.

Wachata pia wameliambia jarida hili kuwa ili mtu aweze kufanya graffiti kiufundi zaidi hata iwe na ubora unaohitajika, ni lazima azingatie mambo haya; ushikaji wa kopo,umbali kati ya msanii na ukuta,kona, kasi ya upulizaji wa rangi(pressure), elevation pamoja na mawazo aliyo nayo aidha ya kiburudani ama kimapinduzi.
Jarida hili pia halikuishia kwa Wachata Crew, liliwatafuta baadhi ya wasanii ambao ni wachoraji wa michoro mingine isiyo ya kigraffiti ili kutaka kujua zaidi sanaa hii ya graffiti wanaichukuliaje?

Jongo ni moja kati ya wasanii wakubwa ambao wamefanya kazi nyingi sana na kuziuza sehemu mbalimbali duniani. Yeye ni mchoraji anayetumia brush, rangi mbalimbali pamoja na canvas kama vitendea kazi vya fani yake hiyo aliyo nayo.

Jongo amesema kuwa pia hufanya graffiti japo si sana, lakini kwa kiasi fulani anaijua sanaa hiyo na ameshawahi kufanya kazi mbalimbali haswa zile za ndani, kwenye kumbi za starehe(club).

Kwa upande wake Jongo amesema kuwa sanaa hii kwasasa ndiyo inazidi kukubalika tofauti na miaka ya nyuma, na kuongeza kuwa japo kuna changamoto nyingi sana anazopata msanii wakati akiwa anachora.
Moja kati ya changamoto hizo ni kama kudharaulika na watu wenye umri kubwa zaidi kwa kudhani kuwa kazi hiyo ya uchoraji wa michoro ya kigraffiti ni ya kiuni jambo ambalo amelikanusha kabisa na kusema kuwa halina ukweli ndani yake.

Changamoto nyingine ni pamoja na ile ya gharama za rangi hizo kuwa kubwa tofauti na rangi nyingine, ambapo yeye alisema kuwa inamuwia vigumu sana msanii kupata ile faida inayohitajika kwani mara nyingi wateja hulalamika bei kuwa juu wakati msanii pia anakuwa ameshatumia pesa nyingi kuzinunua rangi hizo.
Evarist Chikawe pia ni moja kati ya wachoraji waliyopata bahati ya kuongea juu ya mada hii ambapo yeye alikuwa na kazi ya kuelezea jinsi wanavyoipokea aina hii ya sanaa pamoja na jinsi wananchi wanavyoipokea kwa aonavyo.
Katika hilo bwana Chikawe ambaye pia ni msanii maarufu hapa nchini kutokana na kufanya kazi zenye ubora na alizo ziuza katika sehemu mbalimbali ndani na nje ya nchi, yeye amesema kuwa kwa upande wa wasanii wanaipokea sanaa ya graffiti kama sanaa nyinginezo ila yenyewe ikiwa ya kisasa zaidi.

Na kwa upande wa wanunuzi yaani wananchi, bwana Chikawe amesema kuwa nao kwasasa wameanza kuwa na uelewa wa sanaa hii japo imechukuwa muda sana mpaka kuikubalika. Akiongeza katika hilo amesema kuwa mpaka mtindo huo ulipofikia, uliwagharimu sana watu wenye mapenzi nao kwa kuitangaza na hata kutoa elimu kwa jamii na hata kwa wasanii wengine ili waipokee na kuiona kama sanaa nyingine.

Bwana Chikawe amesema kwa hapa nchini watu waliyohusika katika mapinduzi hayo na kuipa jina sanaa hii ya graffiti, ni Bwana Major aliyekuwa pamoja na rafiki yake wakizungu ambao kwa pamoja walifanya workshop mbalimbali pamoja na matamasha ya kutosha ambayo yameisaidia sanaa hii kujulikana na hata kusomeka kwenye ramani ya sanaa zinazofanyika kwenye nchi yetu.

Katibu mtendaji, mstaafu wa Baraza la Sanaa Tanzania (BASATA) 1978-2008, Chief Shogholo Chali naye ametoa mawazo yake kwa kadri anavyoielewa sanaa hii.

Chief Shogholo ambaye pia kwasasa ni Director wa Mikono Art Gallery, amesema kuwa sanaa hii kwake si ya kitambo kwani hata alipokuwa chuoni kwenye miaka ya sabini akiwa akiwa kama mwanafuzi haikuwapo. 

Kwa upande wa graffiti kuwa sanaa kama zilivyo sanaa nyingine yeye pia amekiri kuwa ni kweli nayo ni sanaa katika upande wa uchoraji, ambapo msanii huchukua vitu katika jamii inayo mzunguka na kisha kuviweka akilini ambapo huvitafsiri katika namna ya kisanii na kuvirudisha katika nammna ya michoro ambayo huiweka ukutani.

Katika sanaa hii ya graffiti, katibu huyu mtendaji, mstaafu wa Baraza la Sanaa Tanzania ameonyesha wazi kabisa kutokuwa shabiki nayo kwa kile alichosema kuwa inamdumaza msanii kwani anakosa ule ujuzi wa uchanganyaji rangi kama aliyo nao msanii anayetumia canvas.

Aidha aliongeza kuwa sanaa hii hufanywa na lile rika linalopenda vitu vya chapu chapu na urahisi urahisi ambalo ni la vijana. ”Siipendi sanaa hii kwasababu inarahisisha kazi ya ubunifu ambayo ni sehemu ya sifa ya usanii” aliongeza Chief. 

Pia alisema kuwa sanaa hii inapunguza matumizi ya malighafi asilia ambapo nidhahiri kuwa rangi zitumikazo hazitengenezwi kwa kutumia mimea na malighafi zetu. Kwa kulifafanua hilo zaidi, Chief alisema kuwa alishawahi kufanya utafiti wa rangi asilia akiwa na Profesa Jengo pamoja na bwana Elimo Njau ikiwa ni jitihadaza kupandisha thamani, malighafi zetu katika sanaa ya uchoraji. 

Chief alipo hojiwa na jarida hili juu ya jinsi walivyo ipokea sanaa hii kipindi alipokuwa BASATA, yeye alisema kuwa waliipokea kwa mikono miwili huku wakiichukulia kama ni maendeleo na changamoto ambapo kwa ujumla wake amesema kuwa waliona kama ni wimbi la kuiboresha sanaa ya hapa nchini kwa kuileta katika mtindo wa kisasa zaidi. 

Aidha aliongeza kuwa, japo kuwa sanaa hii inawadumaza wasanii kama alivyo sema hapo awali kwa kushindwa kupata maarifa ya uchanganyaji wa rangi katika michoro yao, lakini hawakuwa na mamlaka ya kuipinga wala kuwakataza vijana kuifanya, kwani nchi yetu ni moja kati ya nchi huria inayompa mtu uhuru wa kufanya biashara yoyote ile isiyo nje ya sheria, tamaduni na maadili yetu. 

Kiongozi huyu wa juu kabisa wa Mikono Art Gallery naye ameungana kimawazo na wasanii wa graffiti na hata wale wasio wagraffiti, juu ya tabia mbovu ya kuitumia michoro hiyo kufikisha jumbe chafu zikiwemo matusi, jambo ambalo alisema kuwa linaweza kuwepo hata kwa wasanii ambao si wanagraffiti.

“Sasa pamoja na kusema kuwa msanii yupo huru lakini hayupo huru kuchinja utamaduni wetu, kwahiyo lazima vyombo vinavyo husika na maendeleo na utamaduni vitoe miongozo itakayolinda heshima, mila na desturi za jamii yetu” aliongeza Chief Shogholo.

Na katika upande wa maoni juu ya sanaa hii Chief amesema kuwa hana vita na wanagraffiti wala malighafi zinazo tumika isipokuwa tu, angetamani kama kungekuwa na uwezekano wa kuifanya kazi hiyo kwa kutumia rangi zetu na kuongeza kuwa wasanii wanapaswa kuzifanya kazi zao kwa kuzingatia mila na desturi huku wakitambua ya kuwa waonaji wakazi zao wapo pia watoto na wangetakiwa wajifunze vitu kutoka kwao vyenye maadili.

0 comments:

Post a Comment